Azania

From Wikipedia

Azania ni jina la kihistoria kwa ajili ya sehemu mbalimbali za pwani la Afrika ya Mashariki. Asili yake ni zamani za Waroma na Wagiriki wa kale.

Mara ya kwanza jina hili limepatikana kwa mwandishi Mroma Plinio Mzee (Gaius Plinius Secundus) aliyeishi wakati wa karne ya kwanza b.K. Kufuatana na maelezo yake Azania ni sehemu zile zilizoanza katika eneo la Adulis (leo: Eritrea) na kuelekea kusini.

Kitabu cha mwongozo kwa ajili ya mabaharia "Periplus ya Bahari ya Eritrea" (karne ya pili b.K.) kinatoa maelezo zaidi zinazoonyesha ya kwamba jina la Azania lilimaanisha pwani la Afrika ya Mashariki kutoka Eritrea hadi Tanzania ya leo.

Mwandishi Cosmas Indicopleustes wa karne ya sita b.K. aliandika Azania ni nchi chini ya utawala wa ufalme wa Aksum.

Katika karne zilizofuata jina la Azania haikutumika tena. Inawezekana ya kwamba sababu yake ilikuwa Waarabu Waislamu walichukua nafasi ya Wagiriki na Waroma wakitawala biashara ya nje ya pwani la Afrika ya Mashariki. Kuna uwezekano ya kuwa Waarabu walitumia jina la "Zanj" kwa ajili ya eneo lilelile.

Katika karne ya 20 jina la Azania limefufuka tena. Nchi huru za Tanganyika na Zanzibar ziliungana tar. 26.04.1964 kuwa Jamhuri ya maungano ya Tanganyika na Zanzibar. Jina jipya lilitafutwa. Hapa jina lile la kihistoria "Azania" lilikumbukwa tena; kwa kuunganisha maneno ya Tanganyika, Zanzibar na Azania jina la nchi "Tanzania" limepatikana.

Kwa namna tofauti jina la Azania lilitumika pia Afrika Kusini. Wakati wa siasa ya Ubaguzi wa Rangi sehemu ya wapinzani wa siasa hii hawakutaka kutumia jina rasmi la "South Africa / Zuid Afrika" tena. Walitafuta jina katika historia iliyotangulia kufika kwa Makaburu wakichukua jina la Azania. Ni hasa vyama vya PAC na Azanian People´s Organization waliotaka kubadilisha jina la Afrika Kusini kuwa Azania. Lakini chama kikubwa cha ANC haikukubali na mipango ilishindikana.