Idhaa ya Kiswahili ya Radio Tehran

From Wikipedia

Idhaa ya Kiswahili Sauti ya Jamhuri ya Kiislamu ya Iran [1] ilianza kurusha matangazo yake kwa mara ya kwanza siku ya Ijumaa usiku ya tarehe 27 Rajab 1415 Hijria iliyosadifiana na tarehe 30 Disemba mwaka 1994 Milaadia. Matangazo ya Radio Tehran yalianza kurushwa kwa muda wa nusu saa tu usiku, na yalifunguliwa kwa mnasaba wa kuadhimisha siku ya kubaathiwa na kupewa Utume, Bwana wetu Muhammad (SAW).

Kwa wakati huo matangazo ya Radio Tehran yaliyokuwa yakirushwa kwa ajili ya nchi za mashariki na katikati mwa Afrika, yalianza yakiwa na wafanyakazi wachache kama vile Sayyid Muhammad Ridha Shushtari, Sayyid Hashim Shushtari ambaye kwa sasa ni marehemu, mabwana Muhammad Baraza, Abdul Fatah Mussa na Ahmed Rashid, Bibi Leila Kimani n.k. Lengo la kuasisiwa Idhaa ya Kiswahili Sauti ya Jamhuri ya Kiislamu ya Iran ni kufikisha sauti ya Mapinduzi ya Kiislamu ya Iran kwa wananchi waliodhulumiwa wa bara la Afrika, kuelimisha na kufichua njama za ubeberu wa kimataifa dhidi ya bara hilo.

Kuanzia tarehe 18 Mfunguo Tatu (Dhulhijja) mwaka 1417 Hijria sawa na tarehe 26 Aprili mwaka 1997 Milaadia, Radio Tehran ilianza kutangaza kwa muda wa saa moja kuanzia saa mbili na nusu usiku kwa saa za Afrika Mashariki, na matangazo hayo kurejewa siku ya pili yake kuanzia saa 12:30 asubuhi kwa majira ya Afrika Mashariki sawa na saa 11:30 asubuhi kwa majira ya Afrika ya Kati. Mnamo tarehe 23 Mfunguo Tatu (Dhulhijja) 1418 Hijria iliyosadifiana na tarehe 21 Aprili 1998 Milaadia, matangazo ya Radio Tehran yalianza kurushwa hewani kwa muda wa masaa matatu katika nyakati za usiku, asubuhi na machana. Saa moja ilikuwa ni marudio ya matangazo ya asubuhi, ambayo yalikuwa yakisikika kuanzia saa saba kamili hadi saa nane kamili mchana kila siku kwa majira ya Afrika Mashariki. Kwa hivi sasa Idhaa imeongeza wafanyakazi wake ambapo matangazo ya mchana nayo sasa yanasikika kwa njia ya moja kwa moja kuanzia saa 5:30 hadi 6:30 mchana kwa saa za Afrika Mashariki. Inarusha matangazo yake kwa ajili ya nchi za Tanzania, Kenya, Uganda, Rwanda, Burundi, Congo, mashariki mwa Zambia, kaskazini mwa Malawi na Msumbiji pamoja na Afrika Kusini. Inarusha pia matangazo yake kwa ajili ya nchi za Mashariki ya Kati hususan za Ghuba ya Uajemi na ina waandishi wake katika maeneo ya Afrika Mashariki na Kati kama vile Kenya, Tanzania, Uganda, Burundi na Kongo.