Ludwig Krapf
From Wikipedia
Johann Ludwig Krapf (11 Januari, 1810 – 26 Novemba, 1881) alikuwa misionari wa kiprotestant wa kwanza Kenya katika karne ya 19 akatunga kamusi ya kwanza ya Kiswahili.
Contents |
[edit] Masomo Ujerumani na Uswisi
Krapf alizaliwa tar. 11.01.1810 katika kijiji cha Derendingen karibu na Tübingen, eneo la Würrtemberg, Ujerumani wa Kusini-Magharibi katika familia ya wakulima wadogo Waluteri. Alisoma shule ya msingi kwake kijijini halafu shule ya sekondari Tübingen. Akiwa mwanafunzi alipenda sana masomo yote yaliyohusu jiografia na lugha. Pamoja na Kilatini na Kigiriki alisoma pia Kifaransa na Kiitalia. Alipokuwa na umri wa miaka 16 alitembelea mara ya kwanza nyumba ya Misioni ya Basel, Uswisi. 1827 – 1829 alijiunga na kozi ya kuandaa wamisionari huko Basel lakini hakupendezwa na maisha ya pamoja akishikwa na wasiwasi kuhusu wito wake akarudi nyumbani na kuingia masomo ya theolojia katika Chuo Kikuu cha Tübingen.
Krapf alimaliza masomo yake mw. 1834. Vituo vya huduma kama mchungaji msaidizi na mwalimu vilifuata. Wakati ule alikutana na misionari aliyempa moyo kurudi Basel.
[edit] Ethiopia 1837-1842
1836 alikutana na mwakilishi wa Church Missionary Society (CMS) aliyemkaribisha kufanya kazi na CMS. Misioni ya Basel ilimpa ruhsa akapokea wito wa kwenda Ethiopia. Krapf alianza mara moja kujiandaa akisoma Ge’ez (lugha ya Kale ya Ethiopia) na Kiamhari (lugha ya kisasa ya Wakristo katika nyanda za juu Ethiopia).
1837-1842 Krapf alifanya kazi ya umisionari huko Ethiopia. Mpango wa misioni ya CMS ilikuwa kuwaamsha wakristo waorthodoksi kwa matumaini ya kwamba watakuwa wenyewe wamisionari bora kwa wenzao wapagani au waislamu. Lakini Krapf hakuelewa vema Ukristo wa kiorthodoksi wa Waamhari. Alishindwa kuelewa maana ya liturgia za ibada na mila na desturi nyingi. Hakuelewa hasa kwa nini wakristo waorthodoksi walisoma Biblia katika lugha ya kale ya Ge’ez hata wasipoelewa lugha hiyo badala ya kutumia utafsiri wa Kiamahari aliyokuwa amefanya.
Hivyo Krapf alijisikia amevutwa zaidi na Wagalla – hii ni jina la zamani za watu wanaojulikana leo kama Waoromo au Borana. Wagalla kwa jumla walikuwa wakifuata dini zao za kiasili, athira za kiislamu zikianza kuonekana. Krapf alijifunza lugha yao alianza kutafsiri sehemu za Agano Jipya katika Kigalla (Kioromo). Mwaka 1842 Krapf alipaswa kuondoka Ethiopia pamoja na wamisionari wengine wa Kiprotestant, akiwa na ndoto ya kurudi na kufanya kazi kati ya Wagalla. Alikaa muda kidogo Kairo / Misri akafunga ndoa, binti arusi alikuwa amemfuata kutoka Ujerumani.
Wakati ule kwake nyumbani Tübingen Chuo Kikuu kilikuwa kimefuata taarifa zake na 1842 alipewa cheo cha Udaktari (PhD) kwa ajili ya utafiti wake katika lugha na historia ya Ethiopia.
[edit] Afrika ya Mashariki 1844-1853
Ethiopia ilikuwa imefunga milango yake hivyo Krapf aliwaza njia nyingine. Alikuwa amesikia ya Wagalla waliwahi kufika hadi pwani za Afrika ya Mashariki. Hivyo Krapf akasafiri Zanzibar kwa lengo kuwafikia Wagalla kupita eneo la Kenya ya leo. Sultani Seyyed Said alimpa ruhsa ya kuanzisha kituo cha misioni huko Mombasa. 1844 Krapf alifika Mombasa akianza mara moja kujifunza Kiswahili pamoja na lugha ya Mijikenda walio wazalendo wa eneo hili. Hapa Mombasa mke na mtoto waliugua Malaria wakafa. Krapf alihamia Rabai iliyoko katika vilima juu ya Mombasa penye joto kidogo akaanzisha kituo cha Rabai Mpya. 1846 misionari mwingine Johannes Rebmann alikuja na kufanya kazi pamoja naye. Hapa Rabai Mpya Krapf alitunga kamusi na sarufi ya Kiswahili ya kwanza.
Krapf na Rebmann walikuwa wazungu wa kwanza walioona milima yenye theluji Afrika. Rebmann aliona Kilimanjaro, Krapf aliona mlima wa Mt. Kenya. Taarifa zao zilipofika Ulaya zilichekwa na wataalamu waliodai milima yenye theluji haiwezekani Afrika. Krapf aliendelea kuwa na matatizo ya kiafya akarudi Ujerumani mw. 1853.
[edit] Urithi wake
Hadi kifo chake aliendelea kuboresha vitabu vyake kuhusu utamaduni na lugha za mataifa mbalimbali ya Afrika. Kwa jumla aliandika kamusi au kutafsiri sehemu za Biblia katika lugha zifuatazo: Ge’ez, Kiamhari, Kioromo, Kiswahili, Ki-mijikenda, Kikamba, Kimassai.
Nyumba yake huko New Rabai imekuwa makumbusho chini ya Museums of Kenya. Jengo la Ubalozi wa Kijerumani huko Nairobi limepewa jina lake.
Krapf alikuwa Mluteri - Kanisa la Kianglikana linamkumbuka kuwa yeye alianzisha Uanglikana Kenya.